Wednesday 3 September 2014

JK: Sera mbaya za ubaguzi chanzo cha ugaidi


NA MWANDISHI WETU
RAIS Jakaya Kikwete amesema moja ya vyanzo vikubwa vya kuzalisha, kulea na kukuza ugaidi duniani ni sera mbaya za ubaguzi zinazowanyima haki za msingi baadhi ya jamii.
Alisema ni muhimu kwa mataifa mbali mbali duniani kubuni na kutunga sera ambazo zinalenga kutoa nafasi na haki za msingi kwa kila mwanajamii na mwananchi kufurahia sehemu ya keki ya taifa.

Rais Kikwete  alisisitiza kuwa  sera za kichumi na kijamii zina mchango mkubwa katika kukabiliana na kupambana dhidi ya ugaidi na vitendo vya msimamo mkali wenye kutumia nguvu na fujo katika nchi yoyote.
Rais Kikwete aliyasema hayo juzi, wakati alipozungumza katika Mkutano wa Wakuu wa Nchi za Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika (AU), uliofanyika kwenye Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Kenyatta mjini Nairobi, Kenya chini ya uenyekiti wa Rais Idrisa Debby wa Chad.
Katika mchango wake kwenye mkutano huo, Rais Kikwete alisema  ni dhahiri kuwa ugaidi ni tishio la kweli  barani Afrika kama ambavyo ripoto ilivyowasilishwa na Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika ambayo ilielezea kwa uwazi  tishio la ugaidi.
“Kwa kuongozwa na ripoti hii, tunatambua sasa kuwa ugaidi ni tatizo gumu sana kwa sababu hakuna nchi duniani isiyoguswa nao na hakuna nchi hata moja duniani yenye uwezo wa kukabiliana nao peke yake. Hivyo ni muhimu kuunganisha juhudi zetu kwenye ngazi zote kitaifa, kikanda, kibara na duniani ili kuweza kukabiliana nao,” alisema Rais Kikwete na kuongeza:
“Kuna maswali mawili muhimu ambayo tunastahili kujiuliza na kuweza kupata majibu mwafaka juu ya kwa nini kuna balaa la ugaidi na jinsi gani tunavyoweza kukabiliana nalo. Katika jitihada zaidi za kukabiliana na tatizo hili ni lazima tutafute kiini hasa cha kujaribu kumaliza ugaidi na vitendo vya msimamo mkali wa kutumia nguvu na fujo. Katika hali hii, sera za kiuchumi na kijamii katika kila nchi zina mchango mkubwa katika mapambano haya.”
Alisema mataifa lazima yabuni na kutunga sera zenye maslahi kwa watu,  ambazo zinalenga kuleta maendeleo na ustawi kwa  wote, sera ambazo hazimbagui yeyote kwa sababu ya kabila lake, dini yake,  ama wilaya ama mkoa atokako.
 “Ni lazima tuwe na sera ambazo kila mwananchi ana haki ya kupata huduma za msingi za kijamii na kichumi na kupata mgawo wao wa haki katika keki ya taifa,” alisisitiza.
Rais Kikwete alisema kuna umuhipi pia kubuni na kutunga sera zinazotoa uhuru na haki za msingi kwa watu wote bila kujali mwelekeo na misimamo yao ya kisiasa.
Hata hivyo alisema wakati mwingine ugaidi unaweza usiwe na mazingira ya kuzaliwa ndani ya nchi kama ilivyotokea kwa ofisi za ubalozi wa Marekani mjini Dar es Salaam na Nairobi zilipolipuliwa kwa mabomu.
“Kikundi cha Al-Qaeda kilikuwa na matatizo na Marekani na kikaamua kuzifanya Tanzania na Kenya uwanja wa mapambano,” alisema.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru