Tuesday 9 September 2014

Wakulima sasa kupewa pembejeo kwa ruzuku

  • Mawakala waliokuwa wakitumia vocha kunywa pombe kitanzini
Na Hamis Shimye
SERIKALI imesema inaanzisha utaratibu mpya wa utoaji wa ruzuku ya pembejeo kwa wakulima na kuachana na utaratibu wa vocha, ambao ulikuwa unafanyika kinyume na utaratibu.
Imesema hali hiyo inasababishwa na ubadhirifu uliokuwa unafanywa na mawakala wasiokuwa waaminifu, ambao walikuwa wanatumia pesa kunywea pombe na malipo kufanya kwa kutumia vocha za pembejeo.
Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Injinia Christopher Chiza, alitoa msimamo huo wa serikali jana, wakati alipokutana na wawakilishi wa benki mbalimbali nchini.
Katika kikao hicho, Waziri Chiza alisema serikali imeamua kuja na mfumo mpya wa kuwawezesha wakulima kupitia vikundi vyao ili waweze kukopa katika benki.
“Lengo tufanye utaratibu huu na kila benki nchini, ambapo wapo walioonyesha nia ya kuanza na sisi katika huu utaratibu mpya, wengine wamesema wataanza mwakani,’’alisema.
Chiza alisema utaratibu wa vocha za pembejeo ulikuwa na matatizo lukuki, ikiwemo mawakala kujinufaisha wao na si wakulima waliokusudiwa na serikali.
Alisema wameshachukua hatua mbalimbali, ikiwemo kuwafungulia mashitaka mawakala wote waliokwenda kinyume, ikiwemo wale waliokuwa wanazitumia vocha kunywa bia.
“Kulikuwa hakuna usimamizi mzuri katika vocha za pembejeo. Utaratibu huu mpya wa mikopo kupitia mabenki utakuwa mzuri na utamnufaisha mkulima,’’ alisema.
Chiza alisema utataribu huo utaanza kutumika muda si mrefu kuanzia sasa baada ya taratibu kukamilika, ikiwemo benki kukubali taratibu zinazotakiwa na serikali.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru