Wednesday 3 September 2014

Mkandarasi Muleba akalia kuti kavu


Na Julieth John, Muleba
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimeiagiza Halmashauri ya Wilaya ya Muleba, kumsimamisha mkandarasi anayejenga miradi ya maji ya Kyota na Katoke kwa kushindwa kukamilisha kazi kwa muda uliopangwa.
Mradi huo wa maji ni miongoni mwa miradi inayotekelezwa kupitia mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN).
Agizo hilo lilitolewa jana na Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Kagera, Costansia Buhiye, wakati alipokuwa akikagua miradi hiyo ambayo ilitakiwa kukamilika  Oktoba, mwaka jana na Mei mwaka huu.
Pia mkandarasi wa miradi hiyo Kampuni ya M/S Sajac Investment ya Dar es Salaam na Dynotech Engineering ya Morogoro, ameshalipwa kiasi cha sh. milioni 837.7 kwa miradi yote miwili kati ya zaidi ya bilioni 1.2.
Awali, Mbunge wa Muleba, ambaye pia ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, alisema kukwama kwa miradi hiyo kunatokana na halmashauri kutoa tenda bila kutangaza wala kushindanisha wakandarasi.
Alisema baadhi ya miradi imekuwa ikitolewa kwa kujuana na hiyo ndio sababu ya kutokamilika kwa wakati.
“Mwenyekiti,  mradi huu wa Kyota ulianza kutekelezwa Aprili 25, mwaka 2013 na ulitarajiwa kukamilika Oktoba 27, mwaka huu, lakini mkandarasi ana visingizo kila kukicha na alishaongezewa miezi minane. Ukiwauliza halmashauri hawajui mkandarasi alipo,” alisema.
Alisema madiwani na viongozi wamekuwa wakiwalea wakandarasi wabadhirifu kwa madai kuwa wakiwasimamisha wataishitaki serikali na kuwataka kuwatumia wanasheria wa halmashauri kusimamia jukumu hilo.
“Huyu mkandarasi ndiye aliyepewa mradi wa Katoke wakati mradi wa Kyota haijakamilika hii ni kutuhujumu,” alisema Profesa Anna.
Kaimu Mhandisi wa Maji wa Halmshauri ya Muleba, Injinia Gilbert Isaac, alikiri mkandarasi wa miradi hizo kuchelewa pamoja na kwamba kampuni hiyo ni ya mtu mmoja licha ya majina kuwa tofauti.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru