Friday 5 September 2014

Serikali ya Tanganyika yakataliwa


Na Peter Orwa, Dodoma
SERIKALI ya Tanganyika imeendelea kupingwa, ambapo wajumbe wa Kamati mbalimbali za Bunge Maalumu la Katiba, wamesema haiwezi kuwa na tija kwa Watanzania.
Kamati nyingi zilizoundwa kwa ajili ya kuchambua Rasimu ya Katiba na ambazo zinawasilisha maoni yake bungeni, zimepinga kuwepo kwa Serikali ya Tanganyika.
Mapendekezo ya kuwepo kwa serikali ya Tanganyika, yamo kwenye Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
UHURU imebaini kuwa tangu kamati hizo zilipoanza kuwasilisha taarifa zake bungeni, imedhihirika karibu zote zilizowasilisha maoni yake kwa upande wa hoja ya walio wengi, hawakubaliani na kuwepo Serikali ya Tanganyika na wamedhihirisha kupitia maoni yao.
Kwa mujibu wa baadhi ya mawasilisho ya juzi jioni na jana asubuhi, sehemu kubwa ya kamati zilipinga uwepo wa serikali hiyo ya Tanganyika.
Akiwasilisha maoni yake juzi jioni, William Ngeleja kutoka Kamati Namba Tisa, alipinga kuwepo fursa ya kuwa na serikali ya Tanganyika, katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Jana, Suleiman Jaffu, msemaji wa Kamati Namba 12, naye alihimiza kuwa katika kamati hiyo, wameafikiana kuondoa Tanganyika na kuwa na Tanzania Bara kama ilivyo sasa.
“Ibara ndogo ya (3) na ya (4) irekebishwe kwa kufuta maneno ‘la Tanganyika’ na kuweka neno ‘Tanzania Bara. ” ilisomeka sehemu ya mawasilisho ya Jaffu kuhusiana na Ibara ya 117 ya rasimu hiyo.
Ibara ya 118 ikisomeka :“Ibara ndogo ya (2) neno ‘Tanganyika’linapendekezwa kufutwa na badala yake lisomeke Tanzania Bara.”
Maoni kama hayo ndio yalijitokeza jana kutoka kwa Juma Lawi, kutoka Kamati Namba Nane, ambayo yalisimama katika hatua zote ikitambua ’Tanzania Bara’ na si Tanganyika.
Kwa upande wake, Dk. Dalali Kafumu, kutoka Kamati  Namba 10, alisema kamati yake imepinga uwepo wa Serikali ya Tanganyika na badala yake itakuwwepo serikali ya Tanzania Bara.
“Rasimu ifanyiwe marekebisho na muundo unaopendekezwa na Kamati yangu ni wa serikali mbili, hautakuwa na Bunge la Tanganyika,” alisema Dk. Kafumu.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru