Tuesday 9 September 2014

Watakiwa kuacha kubweteka, wafanye kazi


NA PRISCA MSHUMBUSI, MWANZA
WAKAZI wa kata ya Mbugani jijini Mwanza, wametakiwa kujitolea ili kujiletea maendeleo badala ya kusubiri kufanyiwa kila kitu na serikali.
Wito huo ulitolewa jana na Mwenyekiti wa
Mtaa wa Mabatini Kaskazini, Ntobi Boniface, alipozungumza na  waandishi wa habari ofisini kwake, ambapo alisema kujituma huleta maendeleo katika jamii.
Alisema kuwepo changamoto hususan katika utengezaji wa barabara za mitaa, ujenzi wa maabara na miradi mingine ya maendeleo, ni kikwazo kwa maendeleo.
“Tuna tatizo la barabara kwa muda mrefu, hali inayosababisha wananchi wakati wa mvua kushindwa kutoka nyumbani, lakini jitihada zinaendelea ili kuboresha mazingira na wananchi wanapaswa kutuunga mkono katika hili,” alisema.
Alisema wamekuwa wakitumia mikutano ya hadhara kuhamasisha jamii kushiriki shughuli za maendeleo ili kukabiliana na changamoto mbalimbali.
Kuhusu hali ya usalama, Boniface alisema ni nzuri na kuwa wananchi wamekuwa wakishirikiana vyema kupitia Polisi Jamii kwa kuwa kila raia ana jukumu la kulinda amani.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru