Wednesday 3 September 2014

Viongozi CHADEMA watifuana kikaoni

Na Chibura Makorongo, Maswa
MBUNGE wa Maswa Magharibi (CHADEMA), John Shibuda, ambaye ametoa notisi ya kuachana na chama hicho, amevurumishiana maneno na mbunge mwenzake, Sylvester Kasulumbayi.
Shibuda na Kasulumbayi, ambaye ni mbunge wa Maswa Mashariki kupitia CHADEMA, waliingia katika mzozo wakati wa kikao cha Baraza la Madiwani la Wilaya ya Maswa mkoani Simiyu.
Mvutano huo nusura uvunje kikao hicho, ambapo Mwenyekiti wa Baraza hilo alilazimika kuingilia kati ili kutuliza munkari.
Hali hiyo ilijitokeza juzi wakati Shibuda aliposimama kuchangia hoja mbalimbali, ambapo aligusa kinachoendelea katika Bunge Maalumu la Katiba na hatua ya kundi la UKAWA kususia bunge.
Pia alisisitiza kauli zake za mara kwa mara kuwa haungi mkono siasa chafu zinazofanywa na UKAWA, ikiwa ni pamoja na muundo wa serikali tatu.
Wakati Shibuda akiendelea kuchangia hoja, Kasulumbayi  alinyoosha mkono na kumtaka Mwenyekiti kumzuia mbunge huyo kuzungumzia masuala ya UKAWA kwa kuwa si mahali pale.
“Mwenyekiti nakuomba umzuie Shibuda aache kuzungumzia masuala ya UKAWA, hapa si mahali pake, ipo sehemu ya kuzungumzia,” alisema mbunge huyo kwa sauti ya ukali.
Hata hivyo, mwenyekiti alimpa nafasi Shibuda kumalizia hoja huku akieleza kuwa, hicho ni kikao cha baraza la madiwani na mbunge ni mjumbe halali, hivyo ana haki kueleza msimamo wake wa kisiasa kwa wananchi waliompigia kura ambao wako Maswa.
Kutokana na kauli hiyo ya mwenyekiti, Kasulumbayi kwa kushirikiana na baadhi ya madiwani wa CHADEMA, walianza kupiga kelele huku wakimtaka Shibuda kutoka wakati madiwani wa CCM wakimshangilia na kupiga kelele huku wakisisitiza kuwa Shibuda amalize muda wake.
Makamu Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Ndila Mayeka, Mkuu wa wilaya hiyo, Luteni Mstaafu, Abdalah Kihato na Mkurugenzi Mtendaji, Trasias Kagenzi, walipigwa butwaa.
Wakizungumza na waandishi wa habari baada ya kikao hicho, wabunge hao kila mmoja alimtupia lawama mwenzake kwa kutokuwa na subira.
Shibuda alimtuhumu Kasulumbayi kuwa hana uvumilivu wa kisiasa na ni mwanasiasa aliyekosa maono.
Kwa upande wake, Kasulumbayi alidai kuwa iwapo Shibuda amechoshwa na CHADEMA, anaweza kwenda anakotaka.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru