Wednesday 3 September 2014

Makame amtolea uvivu Prof. Lipumba


Na Mwandishi Wetu, Pemba
CHAMA cha Allience for Democratic Change (ADC), kimemtaka Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba, asiishie kudai kuvunjwa mkono na polisi,  badala yake akiri kuwa alijiunga na chama hicho kwa lengo kutafuta madaraka na njia ya kuingia Ikulu.
Kimesema kuwa Profesa Lipumba ni mfano wa wanasiasa wenye uchu wa madaraka na kwamba, hakuwa na dhamira ya kujiunga na upinzani, bali ilikuwa kuwania urais.
Hayo yalielezwa na Mkurugenzi wa Uenezi na Habari wa ADC, Ali Makame, wakati akizungumza na Uhuru mjini Wete, Mkoa wa Kaskzaini Pemba jana.
Alisema wakati wana mageuzi wakishiriki na kupigania harakati za mabadiliko ya kisiasa na kidemokrasia, kupata harufu na misikosuko, Profesa Lipumba alikuwa nyuma akiwa ni shabiki na mtumishi wa watawala, lakini kwa sasa anasimama na kupotosha umma kuwa yeye ni mwanamapinduzi.
“Matamshi yake kuwa amevunjwa mkono na polisi ni mbinu za kujikweza kisiasa, anasaka umaarufu  na hakuwa miongoni mwa wanasiasa waliotoa jasho la kupigania mfumo wa  vyama vingi mwaka 1992,” alisema Makame.
Alisema ADC kimeshituka kumsikia kiongozi huyo akilalama mbele ya umma kuwa alipata misukosuko ikiwa ni pamoja na kuvunjwa mkono na polisi jambo ambalo alisema ni uzushi mtupu.
“Profesa Lipumba akisema hivyo, Mapalala, Kasela Bantu, Kasanga Tumbo, Shaaban Mloo na Ali Haji Pandu waseme nini? alihoji na kuongeza kuwa kiongozi huyo wa CUF amedandia treni ya mageuzi kwa mbele kwa lengo la kupata umaarufu,” alisema.
Aliongeza kuwa wakati kundi la wanamageuzi wakipambana na utawala, Profesa Lipumba alikuwa Mshauri wa Uchumi wa Rais Ali Hassan Mwinyi, Ikulu.
Makame alimtaja Mbunge wa Wawi Hamad Rashid Mohamd ndiye aliyemshawishi kiongozi huyo ili ajiunge na CUF, wakati akifundisha Chuo Kikuu cha  Dar es Salaam na hakuonekana kuwa na ndoto ya kushiriki siasa nchini.
 “Maalim Seif anapata mshahara wa SMZ, marupupu na uhakika wa mafao yake milele, Lipumba ana uhakika wa kupata mgawo wa ruzuku kila mwezi, kuwazuia wajumbe wa CUF waisiingie kwenye bunge maalum la katiba na kufinya haki zao si sahihi,” alisema Makame aliyejitoa CUF na kuanzisha ADC.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru