Thursday 17 July 2014

Mlundikano wa kesi wamkera waziri


NA RACHEL KYALA
VITUO vinavyotoa msaada wa kisheria nchini vimetakiwa kupanua wigo wa huduma, ili kuzinusuru mahakama na tatizo la mlundikano wa kesi.


Huduma hizo ni pamoja na kutoa usuluhishi ili mashauri yaishie nje ya mahakama.
Alisema hivi sasa mahakama zimekuwa na mlundikano mkubwa wa kesi, ambazo nyingine zingewezwa na wataalam wa sheria katika vituo hivyo.
Mbali na usuluhishi, vilevile vimetakiwa kuwa na maofisa ustawi wa jamii watakaokuwa wanatoaushauri nasaha licha ya msaada wa kisheria.
Wito huo ulitolewa jana na Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Angela Kairuki alipokuwa akifanya ziara kutembelea vituo hivyo.
“Kuna mahitaji makubwa sana ya msaada wa kisheria katika jamii, hivyo ni vema mkapanua wigo pamoja na kutafiti nini hasa wananchi wanahitaji na namna ya kuwasaidia, kwani kuna uhaba wa wanasheria nchini,” alisema.                                                                                                        Akiwa katika kliniki ya msaada wa kisheria ya Chuo Kikuu Huria Tanzania (OUT), Naibu waziri huyo alipongeza huduma inayotolewa na kituo hicho, kwani kinaunga mkono serikali kuhakikisha wananchi wanapata haki sawa.
Vilevile alisema jitihada zinafanyika ili kuwepo kwa sheria inayosimamia msaada wa kisheria badala ya ile ya mwaka 1961 inayosimamia makosa ya jinai pekee.
Alivitaka vituo hivyo kujikita kutoa mafunzo ya uelewa wa sheria kwa wananchi hususan katika masuala ya ardhi, mirathi, unyanyasaji wa kijinsia kwa wanawake na watoto pamoja na ndoa kwani ndio yenye shida zaidi.
Naibu Wazri huyo pia alikitaka kituo cha Legal Services Facility (LSF), kuhakikisha kinaandaa haraka mpango wa utoaji huduma hiyo kwa njia ya mtandao.
Kituo hicho kina mfuko maalum wa kutoa msaada wa fedha kwa asasi zinazotoa msaada wa kisheria.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru