Monday 21 July 2014

Serikali yakiri baadhi ya watumishi wake bomu


NA MIRIAM SARAKIKYA, EMAGS 
SERIKALI imekiri kuwa baadhi ya huduma zinazotolewa katika sekta ya umma haziridhishi na hazikidhi viwango.
Pia imesema yapo matatizo ya rushwa na ucheleweshaji wa uamuzi kwa watendaji,  bila ya sababu za msingi.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi aliyasema hayo jana, Dar es Salaam, alipokuwa akifungua mafunzo ya siku tatu kwa wakuu wa mikoa na makatibu tawala nchini.
Alisema upo ubabaishaji unaofanywa na baadhi ya watumishi  ambao  wanakiuka maadili katika ngazi za mikoa na serikali za mitaa.
Alisema mikoa inakabiliwa na changamoto za usimamizi kwenye mamlaka za serikali za mitaa ambazo ndio msingi wa kutoa huduma bora kwa wananchi.
Balozi Seif alisema wananchi wanalalamikia huduma zisizoridhisha na zisizokidhi viwango zinazotolewa katika sekta ya umma.
“Wapo wengine hawajiamini katika kutoa uamuzi wa haraka na kusababisha urasimu na ucheleweshaji wa mambo mbalimbali ya maendeleo,” alisema.
Alisema hali hiyo inatokana na kutokuwepo kwa mfumo mzuri wa mawasiliano ya mwingiliano wa kiutendaji baina ya mkuu wa mkoa na katibu tawala.
Balozi Seif alisema wakati umefika, viongozi hao kusimamia umoja, mshikamano, uhusiano na uwajibikaji wa pamoja.
Alisema changamoto ya uhusiano na mwingiliano wa kiutendaji miongoni mwa wakuu wa mikoa na makatibu tawala, zinasababisha baadhi yao kufanya watakavyo.
 Aliwataka viongozi hao kushirikiana na kuaminiana ili kuendelea uhusiano mzuri kazini.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru