Wednesday 25 March 2015

Gari la kitalii lanaswa na shehena ya bangi



NA LILIAN JOEL, ARUSHA
GARI la Kampuni ya Kitalii ya Wengert Windrose, linashikiliwa na polisi kwa tuhuma za kukutwa likiwa limepakiza shehena ya magunia 11 ya bangi.
Gari hilo namba T 695 ARR aina ya Toyota Land Cruiser, likiendeshwa na Frank Faustine, lilikamatwa eneo la Ranch wilayani Longido.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, alisema gari hilo lilikamatwa saa 5:00 usiku na kwamba, bangi hiyo ilikuwa ikisafirishwa kwenda Kenya.
Juzi, wabunge waliibana serikali wakitaka kuwekwa kwa sheria kali ili kudhibiti wimbi la uingizaji na usafirishaji wa dawa za kulevya nchini.
Wakichangia  Muswada wa Sheria ya Dawa za Kulevya, wabunge walipendekeza kuwepo kwa adhabu ya kunyongwa hadi kufa hadharani kwa watakaotiwa hatiani.
Hata hivyo, akiwasilisha muswada huo bungeni, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), Jenista Mhagama, alisema ili kuiongezea ukali sheria hiyo, adhabu kwa watakaokutwa wakitumia au kufadhili dawa za kulevya zimeongezwa na kuwa kali zaidi.
Alisema kifungu cha 12 cha Sheria iliyopo, adhabu ya kujihusisha na kilimo cha mimea ya dawa za kulevya (mfano bangi), inapendekezwa kuwa adhabu yake iwe faini isiyopungua sh. milioni 20 au kifungo kisichopungua miaka 30 au vyote kwa pamoja.
Jenista alisema kosa la kufadhili biashara ya dawa za kulevya, kwa sasa adhabu yake ni faini ya sh. milioni 10 wakati kwenye sheria inayopendekezwa, adhabu ni faini ya sh. bilioni moja au kifungo kisichopungua miaka 30.

“Kwa makosa ya kusafirisha na kufanya biashara ya dawa za kulevya, sheria ya sasa imetoa adhabu ya faini au kifungo cha maisha wakati katika sheria inayopendekezwa, adhabu inayowekwa ni kifungo cha maisha peke yake hivyo, kuondoa uwezekano wa wahalifu kupewa adhabu ya faini ambayo hulipa bila shida yoyote,” alisema.

Alisema sheria inayopendekezwa imeweka adhabu kali zaidi kwa watakaowashawishi au kuwahusisha watoto kujiingiza kwenye matumizi na biashara ya dawa za kulevya na inapendekeza adhabu ya kifungo cha miaka isiyopungua 30 kwa kosa hilo, tofauti na sheria ya sasa ambayo ipo katika eneo hilo.
Tayari wabunge wamepitisha muswada huo na kinachosubiriwa ni kutiwa saini na Rais ili kuwa sheria kamili.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru