Tuesday 3 March 2015

TANESCO sasa mambo shwari Luku




NA EMMANUEL MOHAMED
SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO), limesema tatizo la mfumo wa kununua umeme kwa njia ya mtandao limeshatafutiwa ufumbuzi na kwamba wateja wataendelea kupata huduma hiyo.
Imeelezwa kuwa  licha ya kupatikana kwa ufumbuzi huo, bado mfumo huo utakuwa na kasi ndogo ya kuwahudumia wateja, ukilinganisha  na awali.
Ofisa Uhusiano wa TANESCO, Adrian Mvungi, alisema tatizo hilo linatokana na kutokea kwa hitilafu ya mfumo huo na kusababisha  usumbufu mkubwa kwa wateja o wanaonunua umeme kwa wakala wa vituo vya umeme.
Mvungi alisema juhudi kubwa zilifanywa kumaliza tatizo hilo na kwamba mfumo wa huduma ya kununua umeme kwa njia ya mitandao jana ilianza kufanya kazi.
"Tatizo hili ni la nchi nzima, limewasumbua sana wateja wetu ambao wanatumia huduma ya kununua umeme kwa njia ya LUKU, ikiwemo njia za miamala ya benki, kampuni za simu na kwa njia ya max malipo," alisema.
Alisema kuna wateja ambao walituma pesa lakini hawajapata ‘’tokeni”  za kuingiza kwenye mita, pia wapo waliopata tokeni, lakini hazikubali kuingia, hivyo mfumo haupo katika kasi yake ya awali.
Aidha alisema kutokea kwa tatizo hilo hakuhusiani na mabadiliko ya gharama za umeme kama baadhi ya watu walivyoanza kuzusha kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii.
Mvungi alisema TANESCO, wanatarajia kubadili mfumo wa matumizi ya umeme, utakaokuwa wa kisasa,  tofauti na unaotumika hivi sasa.
"Mfumo huu umepitwa na wakati ukilinganisha na mifumo ambayo inatumika katika nchi zingine,  hivyo TANESCO inatarajia kutumia mfumo mpya kuanzia Aprili mwaka huu, ili kuongeza kasi ya utoaji huduma kwa uhakika na kuondoa usumbufu wa mara kwa mara,"alisema.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru