Tuesday 10 March 2015

Magige Nyerere naye ajitosa kuwania urais



NA KHADIJA MUSSA
MTOTO mwingine wa Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, Magige Nyerere, amejitokeza na kuonyesha nia ya kuwania urais katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba, mwaka huu.
Magige ni mtoto wa pili wa Mwalimu Nyerere kuonyesha nia ya kuwania uras baada ya hivi karibuni Makongoro Nyerere, kutajwa kuwa ni miongoni mwa watu wanaowania nafasi hiyo. 
Mke wa Baba wa Taifa, Maria Nyerere amebariki watoto hao kuwania nafasi hiyo na kusema ni raia halali wa Tanzania na wanayo haki ya kufanya wapendavyo bila ya kuvunja sheria za nchi.
Mama Maria yaliyasema hayo jana nyumbani kwake Msasani,  Dar es Salaam, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ili kuwaondoa hofu wananchi juu ya uzushi kuwa amefariki dunia.

“Makongoro ni mtanzania, naye ameamua kujitosa, anayo haki ya kufanya apendavyo bila ya kuvunja sheria. Magige naye aliniambia anataka kugombea urais nikasema vema,” alisema.

Hata hivyo, alikiri kuwa suala la kuwania urais si jambo dogo, hasa kwa nchi change kwa sababu kuna mambo mengi muhimu ya kuzingatiwa.
Akizungumzia kuhusu kuzushiwa kifo, Mama Maria alisema zilimfurahisha kwa kuwa zilionyesha kuwa shetani ameshindwa, amepata kipigo kutokana na sala na funga anazozifanya.
Hata hivyo, alisema watoto na familia yake walihamaki na kuanza kumpigia simu wakitaka kuhakikishiwa juu ya jambo hilo, ambapo alisema ni moja ya maajabu ya karne ya 21 kwa maerehemu kuongea tena kwenye simu.

“Hakuna kitu kama hicho ni uzushi tu, hasa kinapofikia kipindi cha uchaguzi. Ni mambo ya makundi na hii si mara ya kwanza, watu wanatakiwa kufanya sana maombi kwa taifa ili damu isimwagike,”alisema.

“Nadhani watu walipokuwa hawajaniona UWT, nafikiri hata baada ya kuona mambo yanakwenda hovyo na nipo kimya, wakaona wanishtue,” alisema.

Aliwataja baadhi ya watu waliompigia simu kuwa ni mke wa mtoto wake aliyeko Butiama, ambaye alikuwa amehamaki na kutaka kujua nini kinaendelea. Mwingine ni Musuguri, ambaye alisema aliongea naye huku akiwa anatetemeka.
Alisema uzushi huo, ambao unatokana na masuala ya uchaguzi, uliongeza hofu kwa taifa, hivyo ameona ni bora ajitokeze kwa sababu Watanzania wana hofu na ulimwengu nao una hofu.
Mama Maria ameishauri serikali itenge siku maalumu kwa ajili ya kuliombea taifa.
Katika hatua nyingine, Mama Maria ametaka suala la miiko ya uongozi lizingatiwe kwani hakuna taifa ambalo viongozi wake hawana muongozo wa kimaadili
Alisema kutozingatiwa kwa miiko hiyo ndiko kunakosababisha nyufa kwenye baadhi ya maeneo ya kiutawala na kiutendaji.
Mama Maria pia amelaani mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi (albino) kwa kuwa yanamega furaha ya taifa na kuhoji linakoelekea.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru