Monday 16 March 2015

Uandikishaji BVR Njombe bado tatizo



Na Michael Katona, Njombe
KAZI ya uandikishaji wa daftari ya kudumu la wapigakura kwa Mfumo wa Kielektroniki (BVR) katika mkoa wa Njombe, limeanza rasmi katika kata za Mjimwema, Yakobi na Kifanya.
Hata hivyo, uandikishaji huo umeanza kwa kulalamikiwa na wananchi kwamba unasuasua na kusababisha wananchi wachelewe kwenye vituo, kutokana na mtu mmoja kutumia muda mrefu kujiandikisha.
Mwandishi wa habari hii alitembelea kata ya Mjimwema, katika vituo vya Melinze, Mjimwema, NJOSS, Mpechi na Joshoni na kushuhudia msongamano wa wananchi waliopanga foleni kujiandikisha.
Pia alishuhudia mwananchi mmoja akitumia dakika 20 kuandikishwa,  jambo ambalo lililalamikiwa na wananchi.

"Nipo hapa kwa muda mrefu katika kituo cha Melinze. Nimesimama toka saa 12 alfajiri nikiwahi labda nitaweza kujiandikisha mapema, lakini nilipomwuliza mtaalamu, alisema picha ninayopigwa ni lazima iende makao makuu Dar es Salaam halafu ndiyo kitambulisho kitoke," alisema Maria Sanga mkazi wa Melinze.

Robert Mkongwa, mkazi wa mtaa wa Melenzi, akiwa amejiandikisha alisema ameshuhudia kazi hiyo ikicheleweshwa na tatizo la vidole vyake kukataa kutambuliwa kwenye mashine kisha kurudia zaidi ya mara tatu.

"Kilichonikuta ni uzoefu wa kuchukua taarifa zangu uandikaji ulikuwa taratibu, alama za vitole ziligoma. Nimerudia mara tatu ndiyo zikakubali. Nimetumia  zaidi ya dakika 20 nikiwa ndani mpaka kukamilika na kupata kitambulisho," alisema Mkongwa

Uchunguzi umeonyesha kuwa uandikishaji wa wananchi katika hilo umekuwa ukichukua dakika nyingi baina ya watu watano kitu ambacho kimekuwa kikilalamikiwa na wananchi.
Kutokana na hali hiyo wengine wamekuwa wakiondoka  na kupeana namba za simu kwa ajili ya kupata taarifa kama  foleni imesogea ili aweze kurudi kujiandikisha.

"Mimi nadhani hii kazi itakuwa na changamoto nyingi kwa hapa Njombe. Wataalamu wanaosimamia hii mitambo kwa ajili ya uandikishaji naona wengi hawana utaalamu wa kutosha, maana wamekuwa wakitumia muda mrefu kwa mtu mmoja," alilalamika Said Husein mkazi wa Joshoni.

Akizungumza juzi kabla ya uandikishaji haujaanza, Mratibu wa Uchaguzi Mkoa wa Njombe, Hilmar Danda, alisema mashine 250 zimesambazwa kwa kazi hiyo  huku akiahidi kutojitokeza usumbufu wa msongamano kwa kuwa  kila baada ya dakika tano mtu mmoja angekuwa ameshajiandikisha.

"Zile changamoto zilizojitokeza kule Makambako, tume imejipanga na kuzitatua. Iwapo mashine moja  ingeleta dosari, tatizo hilo tumejipanga kulikabili," alisema Danda.

Mwandishi pia alipita katika vituo vya Mpechi na NJOSS na Mjimwema na kukuta misururu mirefu kwa ajili ya kujiandikisha, ambapo baadhi ya wananchi walilalamikia hali ya kuchelewa kujiandikisha.
"Nipo hapa tangu saa 11 alfajiri kwa ajili ya kuwahi kujiandikisha, lakini huwezi amini mtu akiingia ndani ya kituo anachukua zaidi ya dakika 20 hadi anapotoka. Hii  hali naona inaleta kero sana," alisema Janeth Mligo mkazi wa NJOSS.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru