Thursday 5 March 2015

Ndugai akanusha uvumi wa yeye kuugua



NA MOHAMMED ISSA
BAADA ya kukaa kimya kwa muda mrefu na kutoonekana kwenye shughuli mbalimbali, Naibu Spika wa Bunge, Job Ndugai ameibuka na kusema yupo hai na ni mzima wa afya.
JOB Ndugai
Ndugai ambaye tokea kuanza kwa mkutano wa 18 wa Bunge la Jamhuri ya Muungano la Tanzania alikuwa hajaongoza kikao chochote.
Muda mwingi katika kikao hicho, kilikuwa kikitumia wenyeviti wakati Spika, Anne Makinda, anapokuwa hayupo bungeni.
Akizungumza na Uhuru kwa njia ya simu jana, Ndugai (Kongwa-CCM), alisema amejichimbia jimbo akifanya shughuli za jimbo.
Ndugai alisisitiza kuwa hana tatizo lolote la afya na kwamba ni mzima bali anafanya shughuli za jimbo.

“Nipo huku jimboni na nipo kwa muda mrefu nafanya shughuli zangu za jimbo. Si unafahamu hivi sasa hakuna vikao vya Bunge vinavyoendelea,” alisema kwa sauti ya chini.

Hata hivyo, alisema taarifa zinazosambazwa na baadhi ya watu kama haonekani kwa sababu anaumwa sio za kweli.

“Hizo taarifa zinazosambazwa kama naumwa sio za kweli ni mzima wa afya njema na sina tatizo lolote lile la afya,” alisisitiza.

KATIBU WA BUNGE
Kaimu Katibu wa Bunge, John Joel, alipoulizwa kuhusu kutoonekana kwa Ndugai alijibu kwa ufupi kuwa hizo taarifa kama anaumwa si za kweli.
Joel baada ya muda alituma ujumbe mfupi wa maneno kwenye simu ya muandishi wa habari hizi, ukisomeka hivi ‘Mhe. Ndugai anaendelea na shughuli zake kama kawaida na yuko jimboni na maandalizi ya ziara ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana.
Kinana alianza ziara ya kikazi mkoani Dodoma ambapo ratiba ilionyesha jana alianza na ziara hiyo katika wilaya ya Mpwapwa.
MARA YA MWISHO KUONGOZA VIKAO VYA BUNGE
Ndugai alionekana akiongoza vikao vya Bunge kwa mara ya mwisho, Novemba 20, mwaka jana, wakati wa Bunge lilipokuwa likijadili Ripoti ya Akaunti ya Escrow.
Pamoja na kuwa na kesi Mahakamani lakini Ndugai aliruhusu mjadala huo kujadiliwa licha ya zuio hilo la mahakama.
MATUKIO AMBAYO HAJAONEKANA
Ndugai katika siku za hivi karibuni hajaonekana kwenye baadhi ya matukio yaliyotokea likiwemo la kifo cha hafla cha aliyekuwa Mbunge wa Mbinga Mashariki, Kapteni John Komba, aliyefariki akiwa katika Hospitali ya TMJ, Dar es Salaam, baada ya kujisikia vibaya.
Kifo cha Kapteni Komba kilikutanisha viongozi mbalimbali wa kitaifa, mawaziri, manaibu mawaziri, makatibu wakuu wa wizara za serikali, viongozi wa vyama vya siasa na wadau mbalimbali, lakini Ndugai hakuonekana kwenye msiba, kuaga na maziko.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru