Thursday 12 March 2015

Kinana ashiriki ukarabati wa josho lililoasisiwa na Nyerere


JOSHO la kuogeshea mifugo katika kijiji cha Gwandi, wilayani Chemba, halijafanyiwa ukarabati tangu lilipojengwa mwaka 1969.
Hali hiyo imelifanya jengo hilo kuharibika vibaya na kutakiwa kufanyiwa ukarabati wa kina ili kulirejesha katika hali yake ya kawaida.
Kutokana na hali hiyo, Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, juzi alishiriki katika ukarabati wa jengo hilo, ambalo Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere alishiriki kulijenga mwaka 1969.
Taarifa za uhakika zimeeleza kuwa, jengo hilo halijawahi kufanyiwa ukarabati hadi juzi Kinana alipokuwa akipita eneo hilo wakati wa ziara yake wilayani humo.
“Kwanza nafurahi sana kusikia kuwa jengo hili lilijengwa  na muasisi wa CCM. Nami leo nimefika hapa ili kushiriki ukarabati wa jengo hili,» alisema Kinana.
Alisema josho ni kitu muhimu kwa wafugaji kwani ni lazima iogeshwe mara kwa mara dawa mbalimbali ili kuikinga na magonjwa.
Alisema josho hilo linatarajiwa kuhudumia vijijini vinne vyenye zaidi ya mifugo 14,000, na liko katika hatua za mwisho za ukarabati, ikiwemo kujenga paa jipya, kujenga uzio na kukarabati shimo la kuweka dawa.
Katibu Mkuu aliwataka wakazi wa eneo hilo kuhakikisha kuwa wanalitunza josho hilo ili liwe na faida kwao.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru