Thursday 26 March 2015

Kinana aipongeza NHC


KATIBU Mkuu wa CCM Abdulrahman Kinana, amelipongeza Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), kwa kazi nzuri ya ujenzi wa nyumba pamoja na kutoa mafunzo kwa vijana juu ya ufyatulishaji wa matofali.
Kinana alitoa pongezi hizo  baada ya kuanza kutembelea Jimbo la Vunjo, juzi na kukagua kikundi cha vijana wanaojishughulisha na ufyatuaji wa matofali.
Alisema NHC mbali ya kazi nzuri ya kujenga nyumba kila sehemu, pia imekuwa ikitoa mashine za kufyatulia matofali kwa vikundi mbalimbali vya vijana.
Kinana alisema mpango huo wa NHC umekuwa ukiwasaidia  vijana kwani umewapunguzia  tatizo la ajira kwa kujiajiri na kuuza matofali yao.
Alisema kutokana na vijana kujitokeza na kuanzishavikundi vingi vya ufyatuaji wa matofali hayo ni vyema sasa halmashauri nazo zikawasaidia kwa kuwapa mashine za ziada.
Kwa mujibu wa Kinana  pamoja na kuwapa mashine hizo pia ni muhimu kuangalia uwezekano wa kuwapa zabuni ya kufyatua matofali pale inapotokea halmashauri inahitaji kujenga majengo mbalimbali, ikiwemo shule.
“Sasa vijana hawa wamejitokeza na kunda kikundi chao cha kufyatua matofali, basi na ninyi halmashauri mwangalie uwezekano wa kununua matofali yao pale mnapokuwa mnajenga majengo mbalimbali, kama madarasa na menginyeo, ili kutia  moyo.
“Nampongeza sana  Mkurugenzi wa NHC, Nehemia Mchechu na watumishi wenzake kwa kazi nzuri ya ujenzi wa nyumba,   kwa kutoa mafunzo kwa vijana hawa pamoja na kuwapa nyenzo mbalimbali,’’ alisema.
Alisema si kosa kwa watu wengine nao kuiga mfano wa shirika hilo katika kuwasaidia vijana na makundi mbalimbali kujiondoa katika tatizo la ajira.
Kinana alisema hata hivyo ni vyema vikundi zaidi vya vijana vikaundwa na kuomba msaada wa kupatiwa mafunzo, ikiwa ni pamoja na vifaa kwa ajili ya kufyatua matofali, ili  wajiajiri.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru