Thursday 5 March 2015

TRA yanasa malori ya magendo



NA SAMSON CHACHA, TARIME
UKAMATWAJI wa malori yanayosafirisha mizigo kwa njia ya magendo kutoka Kenya kwa kupitia mpaka Sirari mkoani Mara, umezidi kushika kasi ambapo jana yalikamatwa matatu yaliyosheheni bidhaa mbalimbali zikiwemo nondo na saruji.
Magari hayo yalikamatwa kwa ushirikiano wa Maofisa wa Forodha wa kituo cha Sirari wakishirikiana na wenzao wa kodi za ndani  wilayani hapa.
Akizungumzia tukio hilo, Meneja wa Forodha Mkoa wa Mara, Ben Usaje, alisema magari hayo ni fuso mbili zenye namba T175 BEZ na T385BMQ mali ya Eliya Mangarama, mkazi wa Bunda.
Lingine ni Toyota Hiace namba T556 CLW mali ya Mwita Nyangi, mkazi wa Sirari ambayo yalikuwa yamesheheni saruji, mabomba, nondo, viberiti na chumvi.
Usaje alisema mali hizo zimeingizwa nchini kupitia njia za panya bila ya kulipiwa ushuru kwa nia ya kukwepa kodi hivyo kuikosesha serikali mapato.
Alizitaja baadhi ya njia zinazotumika kuwa ni mipaka ya Kogaja, Kubiterere na Sirari na kwamba, magari na mali zote zimezuiwa hadi hapo wahusika watakapolipa kodi pamoja na faini.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru