Monday 9 March 2015

Okwi aituliza Yanga



NA VICTOR MKUMBO
BAO pekee lililofungwa dakika ya 51 na  Emmanuel Okwi, limeiwezesha Simba kuibuka na ushindi wa bao 1-0, katika mchezo wa Ligi Kuu ulioikutanisha timu hiyo na Yanga.
Okwi alipachika bao hilo kwa shuti kali la mbali baada ya kumchungulia Bartez aliyetoka nje ya lango na mpira huo kujaa moja kwa moja wavuni.
Ushindi huo unaipa jeuri Simba ya kuendelea kuwatambia mahasimu wao ambao wamekuwa wakiibeza Simba baada ya kufanya  vibaya katika baadhi ya michezo yake ya ligi.
Katika mchezo huo, uliofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Simba  ilianza pambano hilo kwa kasi na kuonyesha dalili ya kupata ushindi.
Dakika ya pili Simba ilifanya shambulizi kali kupitia kwa Ibrahim Ajib kabla ya mabeki wa Yanga kuokoa hatari hiyo.
Yanga ilijibu shambulizi hilo dakika ya saba kupitia kwa Simon Msuva, aliyeachia  shuti hafifu lililojaa mikononi mwa kipa Ivo Mapunda.
Timu zote ziliendelea kushambuliana kwa zamu huku Simba ikicheza mipira ya kuotea na kutafuta mabao ya mapema.
Dakika ya 18 nusura Msuva aipatie Yanga bao baada ya kuwachambua mabeki wa Simba na kuachia shuti lililookolewa na beki wa Simba.
Simba ndiyo iliyoonyesha uhai mkubwa kwa kucheza kwa kuelewana na kufanikiwa kutawala mpira kwa asilimia kubwa.
Yanga nayo ilijizatiti na kutafuta nafasi ambapo dakika ya 19, 24, 36 na 41  ilipata nafasi za kufunga kupitia kwa Amis Tambwe, Danny Mrwanda na Mrisho Ngasa, lakini Mapunda na mabeki wake waliondosha hatari zote langoni mwao.
Simba iliendelea kufanya mashambulizi na kutafuta mabao mengine ya kufunga, ambapo dakika ya 80, Okwi alipata nafasi nyingine ya kufunga, lakini shuti alilopiga lilitoka pembeni ya goli.
Hadi mchezo huo unamalizika, Simba ilitoka kifua mbele na kuendeleza rekodi ya kuwafunga wapinzani wao kila wanapokutana.
Katika mchezo huo, mwamuzi Martin Saanya aliwaonyesha kadi za njano Abdi Banda, Juuko Murshid, Haruna Niyonzima, Nadir Haroub na Amis Tambwe baada ya kuwachezea vibaya wenzao.
Simba ilitoka sare ya bao 1-1 na Yanga katika mchezo wa raundi ya kwanza kabla ya kushinda mabao 2-0, katika mechi ya Nani Mtani Jembe.
Simba: Ivo Mapunda, Kessy Ramadhan, Mohamed Hussein, Hassan Isihaka, Juuko Murshid, Abdi Banda, Ramadhan Singano, Jonas Mkude, Ibrahim Ajib/Elias Maguri, Said Ndemla na Emannuel Okwi.
Yanga: Ally Mustafa, Mbuyu Twite, Oscar Joshua, Nadir Haroub, Kelvin Yondan, Said Juma, Simon Msuva, Haruna Niyonzima, Amis Tambwe, Mrisho Ngasa/Sherman na Danny Mrwanda.

Kuna Maoni 0 mpaka sasa.

Toa Maoni Yako Kwa Uhuru